Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Habari

WIZARA YAENDELEZA HAMASA YA UHAKIKI WA TAARIFA ZA ANWANI NA MAKAZI  


Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari imeendelea  kuhamasisha wananchi kuhakiki taarifa zao za  Anwani za Makazi kwa ajili ya kurahisisha zoezi la Sensa ya Watu na Makazi litakalofanyika Agosti 23, 2022.

Kwa nyakati tofauti wananchi waliojitokeza kuhakiki anwani zao  wameeleza kuwa zoezi hilo ni la  manufaa  kwani linawasaidia wao kuweza kujua taarifa zao za makazi endapo zipo sahihi kwenye mfumo.

Kwa upande wake, Mratibu wa  Kitaifa wa Utekelezaji wa Mfumo wa Anwani za Makazi, Mhandisi Jampyon Mbugi alieleza kuwa Mfumo wa Anwani za Makazi ni  msingi wa utambuzi wa maeneo ya makazi, vituo vinavyotoa huduma za jamii na maeneo ya biashara.

Ameeleza kuwa ili mwananchi aweze kuhakiki anwani yake ya makazi, lazima awe anafahamu namba ya nyumba, barabara, mtaa/kitongoji na kata anayoishi. Taarifa hizo, licha ya kuhitajika wakati wa Sensa ya Watu na Makazi, zitakuwa ni taarifa za kusaidia Serikali kupanga na kuboresha mipango ya maendeleo inayokidhi mahitaji kwa kulingana na uhalisia wa idadi ya watu.

Naye mkaazi wa eneo la Chuo cha Mipango, Judith Malongo amesema kuwa “Ni vizuri kwa wananchi wenzangu kuhakiki anwani zao za makazi kwani inawarahisishia makazi yao kutambulika na kufikishiwa huduma kwa urahisi”. Amezitaja huduma hizo kuwa ni pamoja na huduma za zima moto, ndugu na jamaa kufika nyumbani kwa urahisi, kufikishiwa bidhaa au huduma mlangoni (Posta Mlangoni).

Aidha, Bi. Malongo amesisitiza kuwa hamasa hii ya uhakiki wa anwani na makazi ambayo inatumia mifumo ya kielektroniki  inaenda sambamba na  wito wa Serikali wa kuwa na  uchumi wa kidijiti.

Kwa upande wake, Mhandisi Mbugi amelizungumzia zoezi la uhakiki la Anwani za Makazi ni mwendelezo wa utekelezaji  wa Wizara kufuatia maelekezo ya Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa (Mb) ya kuendesha zoezi hilo  na kukamilika ifikapo au kabla ya tarehe 10 Agosti 2022.