Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Habari

WATENDAJI PEMBA WATAKIWA KUONGEZA KASI YA UTEKELEZAJI ANWANI ZA MAKAZI


 

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mohamed Khamis Abdulla (mwenye suti), akikagua nguzo yenye jina la Mtaa wa Chachania katika mkoa wa Kusini Pemba

ZANZIBAR

Watendaji wa Serikali wametakiwa kuongeza kasi ya utekelezaji wa operesheni ya kitaifa ya Anwani za Makazi ili kwa muda uliobakia hadi Mei 22, mwaka huu zoezi la uwekaji wa miundombinu ya Anwani za Makazi liwe limekamilika

Wito huo umetolewa leo Mei 9, 2022 na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mohammed Khamis Abdulla wakati wa ziara yake ya kikazi katika mikoa ya Kaskazini na Kusini Pemba ya kukagua na kuhamasisha utekelezaji wa operesheni hiyo

Amesema kuwa, kazi ya kukusanya na kuingiza taarifa za makazi na wakazi kwenye mfumo limekwenda vizuri na kuwapongeza Mkoa wa Kaskazini Pemba kwa matumizi mazuri ya fedha za Serikali katika zoezi hilo na kuwataka kutumia fedha zilizobaki kiasi cha shilingi milioni 30 kuweka nguzo zenye majina ya barabara na mitaa pamoja na namba za nyumba

Ameongeza kuwa muda wa utekelezaji wa operesheni ya Anwani za Makazi unakaribia kuisha hivyo wanatakiwa kuongeza kasi ya utekelezaji wa opesheni hiyo na ziara yake katika katika mikoa hiyo imelenga kukagua hatua za utekelezaji na kutoa miongozo ya nini kifanyike ili kuweza kuvuka kwa pamoja na kufikia lengo kwa muda uliopangwa

Bwana Abdulla amesisitiza kuwa mfumo wa Anwani za Makazi ni muhimu sana kwa maendeleo ya nchi kwa kuwa utasaidia zoezi la sensa ya watu na makazi na Serikali itaweza kupanga mipango ya maendeleo kulingana na mahitaji, vilevile mfumo huo utasaidia kuboresha utoaji wa huduma nyingine mfano huduma za utalii na usafirishaji wa mizigo na vifurushi kutoka eneo moja hadi jingine

Kwa nyakati tofauti katibu Tawala wa Mkoa wa Kaskazini Pemba Bwana Ali Mohamed Mwinyi na Katibu Tawala wa Mkoa wa Kusini Pemba Bwana Amour Hamad Saleh wamekiri kuwa operesheni hiyo ni miongoni mwa mambo muhimu kwa maendeleo ya nchi na kumuhakikishia Naibu Katibu Mkuu huyo kuwa kabla ya tarehe 18 ya mwezi Mei, 2022 watakuwa wamekamilisha uwekaji wa miundombinu ya mfumo wa Anwani za Makazi katika mikoa yao