Habari
UHAKIKI WA ANWANI ZA MAKAZI WAENDELEA KWA KASI JIJI LA MBEYA

Na Mwandishi Wetu, WMTH, Mbeya
Zoezi la usajili na uhakiki wa taarifa za Anwani za Makazi katika Halmashauri ya Jiji la Mbeya linaendelea kutekelezwa kwa kasi katika kata mbalimbali, likiwa na lengo la kuhakikisha taarifa za makazi ya wananchi zinakuwa sahihi na zilizosasishwa.
Akitoa taarifa ya mwenendo wa zoezi hilo, Afisa Mtendaji wa Kata ya Mabatini, Bi. Emiliana Zambi, alisema kuwa hadi sasa jumla ya nyumba 474 zimehakikiwa na taarifa zake kusasishwa katika kata hiyo.
“Tunashirikiana na wenyeviti wa mitaa katika kuwasiliana na wananchi, jambo linalosaidia kuhakikisha nyumba zote zinahakikiwa kwa usahihi na kwa wakati,” alisema Zambi.
Halmashauri ya Jiji la Mbeya inaendelea kusisitiza wakazi wote kutoa ushirikiano kwa watendaji wanaopita katika mitaa yao ili taarifa zote muhimu za makazi zikamilike kwa ufanisi.