Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Habari

RC MONGELLA AWAKARIBISHA WANANCHI KUSHIRIKI UZINDUZI WA JENGO LA OFISI YA PAPU


Na Faraja Mpina, WHMTH, Arusha

Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe. John Mongella amewakaribisha wananchi wa jiji la Arusha kushiriki uzinduzi wa jengo la Ofisi za Makao Makuu ya Umoja wa Posta Afrika (PAPU) lililopo barabara ya Moshi, mtaa wa Sekei jirani na hoteli ya Mount Meru.

Mhe. Mongela ametoa mwaliko huo leo Septemba mosi, 2023 jijini Arusha ambapo ametoa taarifa ya Mgeni rasmi atakayezindua jengo hilo ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan mnamo tarehe 2 Septemba, 2023.

Ameongeza kuwa ufunguzi wa jengo hilo ambalo Tanzania imeshiriki kulijenga ni uthibitisho tosha wa jitihada za Serikali iliyopo madarakani katika kujipambanua na kuleta mageuzi makubwa katika sekta zote ikiwepo sekta ya habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari.

Katika hatua nyingine, Mhe. Mongella amewataka wananchi wa Arusha kuendelea kuwa wakarimu na kuwakaribisha wageni wetu, wakiwemo Mawaziri kutoka nchi wanachama wa PAPU, Mkurugenzi Mkuu wa Umoja wa Posta Duniani (UPU) Bw. Mesahiko Metoki pamoja wajumbe kutoka nchi wanachama wa PAPU.

Kwa upande wa Postamasta wa Shirika la Posta Tanzania, Bw. Macrice Mbodo amesema Posta ya Tanzania ya Awamu ya Sita sio ile ya kipindi cha baada ya Uhuru kwa sababu imejipambanua kidijitali katika kuhakikisha inawahudumia watanzania.