Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Habari

PAPU KUIKOMBOA AFRIKA KIUCHUMI


Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Nape Nnauye (Mb) amesema Umoja wa Posta Afrika (PAPU) utaweza kulikomboa Bara la Afrika kiuchumi kwa kuwezesha na kurahisisha Biashara Mtandao Barani humo.

Waziri Nape ameyasema hayo tarehe 17 Februari, 2023 alipofanya ziara ya kukagua ujenzi wa jengo la Makao Makuu ya PAPU jijini Arusha. 

“Posta katika Bara la Afrika Imechangia kwa kiasi kikubwa kudai uhuru kwa kusafirisha bidhaa, huduma na hata wakati mwingine kusafirisha silaha zilizotumika katika ukombozi wa Bara letu. Kazi ya kulikomboa Bara ilishakamilika, kazi Iliyobakia ni kulisaidia Bara hili kupiga hatua za kimaendeleo ya kiuchumi.” Alisema Waziri Nape

Waziri Nape ameongeza kuwa ofisi hizo mpya zitakapokamilika ifikapo mwezi Aprili, 2023 zitakuwa na ubora wa kipekee kwa kuwa na ofisi za kisasa na zenye migahawa, sehemu za kuegeshea magari pamoja na kumbi kubwa za mikutano ambazo kwa Tanzania nzima zitapatikana katika jengo hilo la PAPU.

Kwa upande wake naye Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe. John Mongela amepongeza maendeleo ya ujenzi wa jengo hilo ulipofikia na kuahidi kuendelea kutoa ushirikiano kutoka katika ofisi yake mpaka jengo hilo litakapokamilika.

Naye, Katibu Mkuu wa Umoja wa Posta Afrika (PAPU), Dkt. Sifundo Chief Moyo amesema ujenzi wa jengo hilo la grorofa 18  umefikia asimia 94 na litakapokamilika ukiwa juu kabisa utaweza kuona kilele cha Mlima mrefu Barani Afrika, Mlima Kilimanjaro wenye urefu wa 5895m kutoka usawa wa bahari.

Ujenzi wa jengo la Makao Makuu ya Umoja wa Posta Afrika (PAPU) unasimamiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) na linatarajiwa kukamilika mwezi Aprili, 2023.