Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Habari

NAIBU WAZIRI MHANDISI KUNDO AMTUMBUA MENEJA WA TTCL KAGERA, SHIRIKA LA POSTA KAGERA KUCHUNGUZWA


Naibu Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhandisi Kundo Mathew (kushoto) akioneshwa jinsi mfumo wa malalamiko wa huduma kwa mteja wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) unavyofanya kazi katika ofisi za Shirika hilo zilizopo Bukoba Mkoa wa Kagera. Anayemuelekeza ni Afisa wa Shirika hilo Theopista Lwakatare

KAGERA

Naibu Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhandisi Kundo Mathew ametengua uteuzi wa Meneja wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) wa Mkoa wa Kagera Bi. Irene Shayo kuanzia tarehe 30/07/2021 kwa kile kilichobainika kuwa taratibu za uteuzi wake zilikiukwa na utumishi wake umekuwa wa kusuasua, amekuwa akikwepa ziara za viongozi katika eneo lake pamoja na kupika taarifa za mapato na matumizi

Mhandisi Kundo ameyazungumza hayo wakati wa ziara yake ya kikazi katika Mkoa wa Kagera ambapo alitembelea ofisi za TTCL na Shirika la Posta Tanzania (TPC) na kuona kuwa Meneja wa TTCL katika Mkoa wa Kagera hatoshi kuwa katika nafasi hiyo ukizingatia Kagera ni mkoa wa kimkakati kwasababu unapakana na nchi takribani nne hivyo  Meneja wake anatakiwa kuwa na uwajibikaji wenye ufanisi mkubwa

“Ninaagiza Meneja wa Mkoa wa Kagera aondoshwe mara moja katika Mkoa wa Kagera na kuanzia leo asitambulike kama Meneja wa Mkoa wa Kagera, taratibu zifuatwe na apangiwe kazi zingine kulingana na wasifu wake kitaaluma ili aweze kufanya kazi vizuri kwasababu majukumu ya sasa hana uwezo nayo”, alizungumza Mhandisi Kundo

Ameongeza kuwa wao kama Wizara kupitia kwa Waziri mwenye dhamana Dkt. Faustine Ndugulile wana kasi ya kutaka kuona matokeo ya kile ambacho Serikali imedhamiria kukifanya kwa watanzania katika Sekta ya Mawasiliano

Amesisitiza kuwa ili kufanikisha hilo ni wajibu wao kufanya maamuzi ya kuhakikisha taasisi zilizo chini ya Wizara hiyo zinaimarisha mifumo ya utendaji kazi katika ngazi za mikoa na utoaji wa huduma bora zinazokidhi mahitaji ya watanzania

Katika hatua nyingine Mhandisi Kundo alitembelea na kukagua ukarabati wa Ofisi za Shirika la Posta Bukoba zilizogharimu kiasi cha Shilingi Milioni 78,801,000 na kutorudhishwa na kiasi cha fedha kilichotumika kwasababu hakiendani na hali halisi ya ukarabati uliofanywa na kuagiza uchunguzi ufanyike ili kubaini gharama halisi zilizotumika katika ukarabati huo

“Nimetoa maelekezo kwa Mkuu wa Wilaya ya Bukoba Mhe. Moses Machali  aunde kamati itakayohusisha wataalam wa Ujenzi, TAKUKURU na Ofisi ya Usalama wa Taifa (W) ili wakafanye tathmini na kujiridhisha kile ambacho kimefanyika na iwapo ikibainika kuna watu ambao wamefanya ubadhirifu wa fedha za umma watachukuliwa hatua za kisheria

Sambamba na hilo ametoa maelekezo kwa Mkurugenzi Mkuu wa TTCL na PostaMasta Mkuu wa Shirika la Posta kuhakikisha mameneja wao wa Mikoa ambao hawana vigezo na uwezo wa kuongoza Mikoa hasa ile ya  kimkakati wanaondolewa na kuwekwa watu wenye uwezo na vigezo vya kuongoza katika Mikoa hiyo

Mhandisi Kundo yupo katika ziara ya kikazi katika Mkoa wa Kagera kwa ajili ya kukagua miundombinu ya mawasiliano na upatikanaji wa huduma za mawasiliano ambapo ametembelea katika wilaya ya Muleba, Bukoba na Misenyi na amepanga kuendelea katika Wilaya za Kyerwa, Karagwe na Ngara. Ziara yake katika Mkoa huo ilianza tarehe 29 Julai hadi tarehe 2 Agosti 2021