Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Habari

MSIMAMO WA NCHI NI KULINDA UHURU WA VYOMBO VYA HABARI


Na Lilian Lundo - WHMTH

Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Nape Nnauye amesema msimamo wa thabiti wa nchi ya Tanzania ni kulinda Uhuru wa Vyombo vya Habari, na ndio maana Serikali iliamua kufanya marekebisho ya Sheria ya Huduma ya Habari Sura ya 229, ili ikidhi uhuru wa vyombo vya habari.

Mhe. Nape amesema hayo leo Julai 31, 2023 jijini Dar es Salaam alipokuwa akifungua Kozi Fupi ya 15 ya Wahariri wa Vyombo vya Habari inayotolewa na Chuo cha Taifa cha Ulinzi.

“Wanahabari niwahakikishieni msimamo thabiti wa nchi yetu ni kulinda Uhuru wa Vyombo vya Habari. Mhe. Rais mara nyingi amekiwa akiagiza kufanya kazi bila kuingilia uhuru wa Vyombo vya Habari,” amesema Mhe. Nape.

Aidha amewataka Wahariri hao mara watakapomaliza kozi hiyo na kurudi katika vituo vyao vya kazi, wafanye kazi kwa kuangalia maslahi ya nchi, vilevile amewataka kuendelea kulifanya Taifa kuwa kitu kimoja na kukuza umoja wa Taifa.

Kwa upande wake Kansela wa Chuo cha Taifa cha Ulinzi, Dkt. Abdulhamid Yahya Mzee amesema kuwa mafunzo hayo kwa Wahariri wa Vyombo vya Habari yataleta matokeo chanya kwa washiriki hao na kufanya Taifa lisonge mbele.

Naye, Mkuu wa Chuo cha Taifa cha Ulinzi, Meja Jenerali Ibrahim Mhona ametaja kauli mbiu ya mafunzo hayo kuwa ni “Nafasi za Vyombo vua Habari Katika Kuimarisha Usalama na Kukuza Umoja wa Kitaifa”.

“Kupitia kozi hii ya kimkakati, tunaenda kuona Wahariri ambao wataenda kufanya kazi ya uhariri wa kimkakati kwa kizingatia maslahi ya nchi yetu,” amesema Meja Jenerali Mhona.

Ametaja baadhi ya maeneo ambayo washiriki hao watafundishwa kuwa ni, Dhana ya Usalama wa Taifa, Maslahi ya Nchi, Masuala ya TEHAMA na thari zake pamoja na Wajibu wa Mhariri.