Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Habari

MNARA WA TBC MAKETE KUTATUA CHANGAMOTO YA USIKIVU


Na Immaculate Makilika – MAELEZO, Makete

Naibu Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Mhandisi Kundo Mathew amekagua mradi wa ujenzi wa mnara wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) ulipo katika Kijiji cha Usungilo walayani Makete ambao utajwa kuwa baada ya kukamilika kwake utatatua changamoto ya usikivu wa matangazo ya TBC wilayani humo.

Akihutubia wananchi jana kijijini hapo mara baada ya kukagua mradi huo, Mhe. Naibu Waziri Kundo amesema kuwa mradi huo ni muhimu kwa vile utawapa wananchi taarifa mbalimbali kuhusu utekelezaji wa shughuli zinazofanywa na Serikali sambamba na fursa za biashara.

“Mhe. Rais Samia ameamua kuleta takribani shilingi milioni 450 kwenda kwenye huu mnara, na utakapokamilika mtaweza kusikiliza matangazo ya TBC FM na TBC Taifa hivyo kupata taarifa kuhusu kazi zinazofanywa na Serikali yenu ikiwemo uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali, mfano katika bajeti ya mwaka 2022 tuna miradi mingine yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni moja itajengwa Makete baada ya kuombwa na Mbunge wenu”. Amesisitiza Mhe. Naibu Waziri Kundo.

Ameongeza kuwa baada ya kukamilika kwa mnara huo wa TBC kutasaidia vituo vya redio vya Green fm na Kitulo kuweka vifaa vyao ambavyo vitasaidia kuongeza usikivu wilayni Makete.

Mkuu wa Kanda Ziwa Nyasa wa TBC, Noela Njawa amesema kuwa mradi huo wa ujenzi wa chumba cha mitambo na jenereta mnara unalenga kuongeza usikivu wa matangazo ya redio ya TBC kwa wananchi.