Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Habari

MIPAKANI KUPATA HUDUMA ZA MAWASILIANO KIUWAKIKA- WAZIRI NAPE


Na Chedaiwe Msuya. WHMTH


SERIKALI imezindua mnara wa Huduma za mawasiliano katika kijiji cha katuka kata ya msanzi wilayani Kalambo mkoani Rukwa wenye Thamani  zaidi ya Millioni 300 kwa lengo kufikisha huduma za mawasiliano kwa wananchi.

Akizindua Huduma ya mawasiliano katika Kata ya Msanzi , Waziri wa Habari Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhe. Nape Nnauye (Mb)  akiwa katika ziara yake mkoani Rukwa amesema ziara yake ya kukagua shughuli za mawasiliano hasa kwenye ukanda wa mipaka ni Maagizo ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kuhakikisha mikoa yote ya mipakani inapata huduma ya mawasiliano ya uhakika .

"Rais Dk. Samia Suluhu Hassani ameagiza Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari kuhakikisha mikoa yote ya mipaka wananchi wanapata huduma ya mawasiliano ya uhakika ili waache kutumia mawasiliano ya nchi jirani" Amesema waziri Nape

Aidha, Waziri Nape ameishukuru kampuni ya mawasiliano Tigo kwa kushirikiana na serikali kukubali kupeleka Mnara katika kijiji cha katuka.

"Tigo wamefanya kazi nzuri sana na kwa hali ya kawaida wao peke yao wasingeweza kuja kwa sababu kibiashara mnara kujengwa hivi hivi tu usingelipa maana wao wanajenga minara kkatika maeneo yenye biashara kubwa na yenye watu wengi ili huduma zirudishe gharama za ujenzi na kilichofanyika serikali chini ya Rais Dkt Samia ilianzisha huduma ya mfuko wa mawasiliano kwa wote ikatenga fedha na Rais akasema pelekeni huduma ya mawasiliano kijiji cha katuka" Amesema waziri Nape

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Queen sendiga amesema kupitia huduma ya Mnara wa mawasiliano katika kijiji cha utaingiza kiasi cha shillingi Millioni Tatu(3) kwa Mwaka ambapo ameutaka uongozi wa kijiji  kutumia fedha hizo kwa maendeleo ya kijiji na siyo kutumia fedha hizo kugombana wenyewe kwa wenye bali wazielekeze fedha hizo kwenye maendeleo na siyo kwenye mifuko yao binafsi.

"Viongozi wa kijiji hiki mkae kwa pamoja kujadiliana kwa maandishi na Muktasari kwamba fedha hizo zitumike kwa maendeleo ya kijiji na siyo muishie kugombana,pia Mtendaji wa kijiji nakutaka kila unaposoma mapato na matumizi ya kijiji hiki uingize pesa hii wananchi waifahamu maana kuwasomea wananchi mapato na matumizi ni suala la kisheria" Amesisitiza Mkuu wa mkoa wa Rukwa Queen Sendiga

Nao baadhi ya wananchi waliohudhuria uzinduzi huo akiwemo Bw. Petro Kisanga wameishukuru serikali ya Rais Dk samia suluhu Hassan kwa kupeleka huduma ya mawasiliano katika kijiji chao ambapo wamesema hawatotumia tena huduma za nchi jirani bali watatumia huduma waliyoletewa.


Ziara ya Waziri wa Habari Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Nape Nauye Mkoani Rukwa  ni Maagizo ya Rais Dk samia suluhu Hassan kuhakikisha mikoa yote ya mipakani inapata huduma ya mawasiliano ya uhakika ili Watanzania watumie mawasiliano ya ndani ya nchi na siyo kutumia mawasiliano ya nchi jirani.