Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Habari

WIZARA YASAINI MAKUBALIANO YA KUBORESHA BUNIFU NA KAMPUNI CHANGA NCHINI


Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari na Kampuni ya Tanzania Startups Association (TSA)  imesaini makubaliano ya ushirikiano wa kuanzisha na kuimarisha miongozo mbalimbali inayosimamia bunifu na kampuni changa nchini (startup’s policy)

Akizungumza baada ya kusaini makubaliano hayo leo Februari 14, 2023 jijini Dodoma, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dkt. Jim Yonazi amesema lengo ni kuhakikisha kampuni changa na bunifu zinakuwa na mazingira bora ya kiutendaji pamoja na kulifikia soko la bidhaa wanazozalisha.

“Tunaenda kutengeneza mazingira bora ya kisera na kisheria ili kuhakikisha yale yanayofanywa na kampuni changa (startup) yanachagiza mipango ya kitaifa ya maendeleo na kushiriki kukuza uchumi wa nchi”, amezungumza Dkt. Yonazi

Aidha Dkt. Yonazi amezungumzia mikakati iliyopo ya kuhakikisha TEHAMA inakuwa nguzo muhimu kwa vijana kujikwamua kiuchumi kwa kuanzisha kampuni changa na bunifu mbalimbali na kutatua changamoto za ajira pamoja na kuzifikia fursa za masoko zilizopo ndani na nje ya nchi.

Kwa upande wa Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya TSA, Bw. Zahoro Muhaji amesema kampuni hiyo inamilikiwa na wanachama na ipo kama mwamvuli wa startups zote nchini

Amesema kuwa kampuni changa na bunifu mbalimbali zitakuwa na manufaa zaidi katika nyakati zijazo kwa kuzingatia kwamba asilimia kubwa zinatumia TEHAMA hivyo zitachangia kukuza uchumi wa kidijiti.

“Kuna uwezekano mkubwa wa kampuni changa yaani startups kuchangia kukuza pato la Taifa na kutengeneza ajira wa wastani wa ajira 70 kwa kila startups”, amesema Muhaji

Naye Mkurugenzi wa Uendelezaji wa Mifumo ya TEHAMA wa Wizara hiyo, Bw. Mulembwa Munaku amesema kuwa makubaliano hayo yanaenda kufungua fursa kwa vijana kuweza kusaidiwa zaidi katika bunifu zao na kuchochea ajira kwa kutumia TEHAMA.