Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Habari

MABADILIKO YA KIDIJITALI KUFUNGUA FURSA MPYA SHIRIKA LA POSTA


Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhe. Dkt. Faustine Ndugulile ameliagiza Shirika la Posta Tanzania (TPC) kwenda sambamba na mabadiliko ya teknolojia ili kuendesha Shirika hilo kisasa zaidi na kutafuta fursa mpya za kufanya biashara kwa ustawi wa Shirika hilo.

 

Dkt Ndugulile ameyazungumza hayo wakati akifunga kikao kazi cha Menejimenti na Mameneja wa Shirika hilo kilichofanyika kwa muda wa siku tatu jijini Dodoma kwa ajili ya kujadili utekelezaji wa majukumu ya Shirika katika ngazi ya Mkoa.

 

“Hatuwezi kuendesha Shirika la Posta kama tulivyokuwa tunaendesha miaka ya nyuma, lazima twende sawa na mabadiliko ya TEHAMA na mahitaji ya sasa ya Dunia yanataka nini, ndio tafsiri ya kauli yangu ya msipobadilika mtabadilishwa na mazingira”, Dkt Ndugulile

 

Aliongeza kuwa kila mkoa una aina tofauti ya fursa na kuwaagiza mameneja wa mikoa waende kuziangalia fursa hizo ili kulibadilisha Shirika hilo kuwa moja ya taasisi zenye mapato makubwa na kuwa na mchango mkubwa katika Taifa.

 

Aidha, ameliagiza Shirika hilo kuhakikisha ifikapo Juni 30 mwaka huu Vituo vya kutolea huduma Jumuishi za uwakala wa taasisi za Serikali “one stop centre” viwe  vimeanza kutoa huduma katika ofisi za Shirika hilo na kuwaagiza watendaji wa Wizara kufanya ufuatiliaji huku Postamasta Mkuu na idara ya masoko ya Shirika hilo kufanya kazi ya kutafuta fursa mpya za biashara.

 

Katika hatua nyingine Dkt Ndugulile amezungumzia ugeni wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Posta Afrika (PAPU) Younouss Djibrine alipotembelea ofisi za Wizara hiyo zilizopo Mji wa Serikali Mtumba , ambapo pamoja na mambo mengine amezungumzia pia ujenzi wa Makao makuu ya Umoja wa Posta Afrika (PAPU) unaoendelea  jijini Arusha,  na kutoa rai kwa Shirika la Posta Tanzania kuwa kielelezo na mfano wa utoaji wa huduma za Posta Afrika.

 

Naye Katibu Mkuu wa PAPU Younouss Djibrine ambaye alishiriki katika ufungaji wa kikao kazi hicho amesema kuwa fursa nyingi zinapatikana kutokana na mabadiliko ya teknolojia ya dijitali kwa kutumia vifaa vya TEHAMA kuboresha huduma za posta na kusisitiza suala la ubunifu kuwa ni suala la msingi katika kufikia mafanikio ya Shirika hilo.

 

Awali Postamasta Mkuu wa TPC Hassan Mwang’ombe alisema kuwa kikao kazi hicho kimejiwekea maazimio ya pamoja ya kwenda kufanyia kazi ili kuhakikisha Shirika linafikia malengo yake ya kuhudumia wananchi na kuimarisha mapato ikiwa ni pamoja na kutafuta fursa mbalimbali za kufanya biashara na taasisi mbalimbali za Serikali.

 

Aidha, pamoja na mambo mengine, Dkt Ndugulile aliwakabidhi Mameneja wa Mikoa vitendea  kazi ambazo ni kompyuta mpakato 24 vilivyonunuliwa na Shirika hilo kwa ajili ya kuwarahisishia Mameneja hao kutimiza majukumu yao katika vituo vyao vya kazi.