Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Habari

KUNDO AFUNGUA MKUTANO WA 41 WA BARAZA LA UTAWALA LA PAPU.


Na Faraja Mpina, WHMTH, Arusha

Naibu Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Mhandisi Kundo Mathew, amefungua Mkutano wa 41 wa Baraza la Utawala la Umoja wa Posta Afrika (PAPU) unaofanyika kwa siku mbili, jijini Arusha.

Mkutano huo unaofanyika Agosti 29 na Agosti 30, 2023 umejikita katika kujadili na kupanga mikakati ya kuhakikisha Sekta ya Posta Barani Afrika kupitia Umoja wa PAPU unabadilisha mfumo wa kiutendaji kwenda kidijitali.

Akizungumza katika ufunguzi wa Mkutano huo, Mhandisi Kundo amewahakikishia wajumbe wa Mkutano huo kuwa nchi ya Tanzania itaendelea kutoa mchango wake katika Umoja huo kama mwanachama na Mwenyeji wa Makao Makuu ya PAPU ikiwa ni pamoja na kuchangia rasilimali watu na rasilimali fedha.

Amesema kuwa nchi ya Tanzania tayari imepiga hatua katika kutoa huduma za posta kidijitali ambapo utekelezaji wake ulianza kwa Serikali ya Tanzania chini ya Mhe. Rais Samia kuwekeza katika ujenzi wa miundombinu ya kidijiti.

Mhandisi Kundo ameitaja miundombinu hiyo kuwa ni Mfumo wa Anwani za Makazi, Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano, Minara ya Mawasiliano, mradi wa kupeleka intaneti majumbani (fiber to home) pamoja na kufunga internet kwenye maeneo ya wazi.

“Mikutano kama hii inalileta Bara la Afrika pamoja na katika maendeleo ya sekta ya posta hatutaki kuachana nyuma, mfano Nigeria wapo katika hatua fulani, Kenya wapo hatua fulani, Uganda wapo hatua fulani, tunataka tutembee pamoja katika mabadiliko ya kidijiti ili kuhakikisha mazingira yote ya kiutendaji yanaendelea kulingana hivyo kurahisisha utoaji wa huduma”. Amesisitiza Mhandisi Kundo.

Kwa upande wa Mwenyekiti wa Baraza la Utawala la PAPU aliyemaliza muda wake, Bw. Richard Ranarison kutoka Madagascar amesema PAPU inathamini mchango mkubwa wa Serikali ya Tanzania kwa kuwa nchi mwenyeji wa Umoja huo ambapo jengo la ofisi ya Makao Makuu ya Umoja huo linatarajiwa kuzinduliwa Septemba 2, 2023 na litakuwa kitovu cha mabadiliko ya kidijitali katika Sekta ya Posta Barani Afrika.

Naye Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Bw. Selestine Kakele amesema Umoja wa PAPU ni injini ya mabadiliko ya Sekta ya Posta Barani Afrika.

Amesema kuwa, Mkutano wa Baraza la Utawala ulitanguliwa na vikao vya kamati tendaji za wataalamu wa Baraza hilo ambazo zilijadili kwa kina masuala mbalimbali ya kuboresha Sekta ya posta Afrika.

Mkutano huo wa 41 wa Baraza la Utawala la PAPU umefanya uchaguzi wa Mwenyekiti wa Baraza hili ambapo Bi. Tshibonge Mbiye Sandra kutoka Jamhuri ya Kongo, DRC amekuwa mwenyekiti mpya wa Baraza hilo akichukua nafasi ya Bw. Richard Ranarison aliyemaliza muda wake.