Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Habari

JAMII NAMBA KUCHOCHEA UCHUMI WA KIDIJITALI ZANZIBAR


Kwa kuzingatia umuhimu wa TEHAMA na lengo la serikali la kuwa na serikali mtandao, Mkurugenzi wa Idara ya Uendelezaji Mifumo na Huduma za TEHAMA (DISDS) Bw.Mohammed Mashaka amesema kuna hitajio kubwa la kuwatambua wale wote ambao wanapewa huduma ili kuendana na kasi ya mabadiliko ya sayansi na Teknolojia.

Kauli hiyo imetoleo leo August 8.2023 na Mkurugenzi huyo katika kikao kazi cha kutoa uelewa kwa wadau wa Zanzibar kuhusu Mradi wa Huduma Pamoja na uanzishwaji wa Mfumo wa Utambuzi wa Kidijitali kwa kutumia Jamii Namba ambapo amesema kuna haja ya kuwa na namba moja ya kumtambua anayepokea huduma za serikali.

Aidha,Bw. Mohammed amesema kwenye utoaji wa huduma kwa wananchi hakuna mipaka,hivyo serikali inatoa huduma na sekta binafsi zinatoa HUDUMA lengo ni kuhakikisha tunawatambua wale wote ambao wanapokea huduma na italeta urahisi katika kuwatambua.

"Mwananchi anayetokea Magu Bara kule anakuja chakechake Pemba anataka huduma za serikali, lazima aweze kutambulika maana sisi tupo ndani ya mpaka wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania". amesema Bw. Mohammed.

Kwa upande wake  Mratibu wa Mradi wa Tanzania ya Kidijitali, Bw.Bakari Mwamgugu ametaja faida za Mfumo wa Utambuzi wa Kidijitali kwa kutumia Jamii Namba ni pamoja na kuhifadhi taarifa mbalimbali za kijamii ikiwemo Ardhi,Afya pamoja shuleni.

"Mfano mtoto anapozaliwa lazma awe na hiyo Namba jamii ambayo itamsaidia akiwa anafanya taratibu za Afya atatumia namba hiyo,na anapo sajiliwa shule mpaka chuo huko atatumia namba hiyo mpaka kifo chake". Amesema Bw. Bakari.

Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari na Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi Unguja, pamoja na Taasisi zake Zanzibar wanaendelea na kikao kazi cha kutoa uelewa kwa wadau wa Zanzibar kuhusu Mradi wa Huduma Pamoja na uanzishwaji wa Mfumo wa Utambuzi wa Kidijitali kwa kutumia Jamii Namba.